KATIBU MKUU NYAMHANGA AAGIZA UJENZI MIZANI BARABARA YA DODOMA – BABATI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga, akitoa maelekezo kwa mkandarasi wa kampuni ya CHICO anayejenga sehemu ya barabara ya Mayamaya – Mela (km 99.35), alipofanya ukaguzi mkoani Dodoma.

 

Mhandisi Mshauri wa barabara ya Mayamaya – Mela (km 99.35), Eng. Leornado Licari, akitoa maelezo ya mradi wa barabara hiyo kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga (wapili kushoto), alipofanya ukaguzi mkoani Dodoma.

 

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga, amewaagiza Mameneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mikoa ya Dodoma na Manyara kuhakikisha wanatafuta eneo la kujenga kituo cha mizani ili kudhibiti madereva wanaozidisha uzito katika barabara ya Dodoma- Babati (km 263), inayojengwa kwa kiwango cha lami.
Akizungumza katika eneo la Bonga, mkoani Manyara Eng. Nyamhanga, alisema barabara hiyo ambayo inatarajiwa kukamilika baadae mwezi huu inahitaji uwepo wa mizani kwa haraka ili kudhibiti magari yanayozidisha uzito na kuharibu barabara.

“Hakikisheni mnatafuta eneo la kujenga mizani ndani ya miezi miwilli ambapo wakandarasi bado wapo hapa ili iwe rahisi kwenu kumtumia mmoja wa wakandarasi hawa kuweza kujenga kituo hiki haraka, uwepo wa mizani hii utasaidia kudhibiti magari makubwa yanayozidisha uzito”, amesema Katibu Mkuu Nyamhanga.
Aidha, Eng. Nyamhanga amewaagiza mameneja wote nchini kuchukua hatua kali za kisheria kwa watu wote wanaopitisha mifugo katika barabara ili kudhibiti uharibifu wa barabara.

Amewataka madereva wote nchini kuendesha magari yao kwa tahadhari na kuzingatia alama za barabarani ili kudhibiti ajali zinazoepukika. Katibu Mkuu Nyamhanga ametoa wito kwa wananchi wanaoishi kando ya barabara hiyo kuhakikisha wanatumia fursa ya kukamilika kwa barabara hiyo kwa ajili ya kuleta maendeleo katika maeneo yao ili kukuza uchumi kwa familia zao na Taifa kwa ujumla.
Amemataka mkandarasi wa sehemu ya barabara ya Mela – Bonga (km88.8) kuhakikisha anakamilisha kazi zilizobaki kwa wakati na kwa viwango vilivyo kwenye mkataba. Katika hatua nyingine, Eng.Nyamhanga, ametembelea na kukagua barabara ya Mayamaya- Mela (km 99.35) kwa kiwango cha lami na daraja la Kelema lenye urefu wa mita 205 na kuridhishwa na ujenzi wake na kumtaka mkandarasi wa mradi huo kukabidhi mradi huo ifikapo mwezi Oktoba mwaka huu.
Kwa upande wake, Mhandisi Mshauri wa barabara ya Mayamaya- Mela (km 99.35), Leornado Licari, amemhakikishia Katibu Mkuu huyo kumaliza mradi huo kwa wakati kwani kazi zilizobaki kwa sasa ni ndogo kama kumaliza tabaka la mwisho la lami na uwekaji wa alama za barabarani.
Barabara ya Dodoma- Babati (km 263) ni sehemu ya barabara kuu ya kaskazini (Great North road), inayoanzia Capetown nchini Afrika Kusini hadi Cairo nchini Misri ambapo hapa nchini barabara hiyo inayopitia Tunduma mkoani Mbeya, hadi Namanga mkoani Arusha ina urefu wa kilomita 1500,hivyo kukamilika kwa sehemu ya barabara ya Dodoma – Babati (km 263), kunaiunganisha barabara yote kutoka Capetown hadi Cairo yenye urefu wa kilomita 100000 kwa kiwango cha lami.

 

Muonekano wa sehemu ya juu ya daraja la Kelema lenye urefu wa mita 205 linalounganisha wilaya ya Chemba na Kondoa mkoani Dodoma.

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Eng. Joseph Nyamhanga, akikagua kingo za daraja la Kelema lenye urefu wa mita 205 linalounganisha wilaya ya Chemba na Kondoa mkoani Dodoma.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.